LONGOPA AMTAKA MKANDARASI MWANZA KUKAMILISHA MRADI KWA WAKATI

Imewekwa: 21 May, 2022
LONGOPA AMTAKA MKANDARASI MWANZA KUKAMILISHA  MRADI KWA WAKATI

Na Mwandishi Wetu

 Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali,   Dkt. Evaristo  Longopa amemtaka  Mkandarasi anayejenga   Jengo  la Ofisi ya Mwanasheria  Mkuu  wa Serikali Mkoani Mwanza , kuhakikisha  anajenga kwa viwango  vinavyokubalika na kwa  wakati.

Ametoa msisitizo huo  siku ya Ijumaa wakati alipotembelea, kukagua  na kuzungumza  na Mkandarasi na kujionea kazi mbalimbali zinazoendelea katika eneo la mradi Buswero .

Akiwa katika eneo hilo,  Dkt. Longopa  pamoja na kumtaka mkandarasi  kuzingatia viwango na muda wa mradi pia ameelezea kuridhishwa kwake na namna  Mkandarasi  huyo SUMAJKT alivyoanza kazi.

Katika maelezo yake kwa  Naibu Mwanasheria Mkuu  Dkt. Longopa, Mkandarasi  pamoja na mambo mengine ameahidi kuukamilisha mradi huo kwa wakati ambao ni  Miezi 18, kwa kuzingatia mkataba na kwa viwango. 

Jengo    OMMS mkoani  Mwanza  ni  jengo ambalo ujenzi wake   unagharamiwa na  OMMS   kwa  gharama ya  shilingi  Bilioni  Tatu hadi kukamilika kwake. 

Aidha  Jengo hili la Mwanza   lenye ghorafa  tatu (3)litakuwa Jengo la Kwanza la   Kituo  Jumuishi  chini ya  usimamizi wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali litakalotumiwa na  Ofisi ya Mwanasheria Mkuu, Ofisi ya Wakili Mkuu na  Ofisi ya Taifa ya Mashtaka

Baadhi ya kazi ambazo zimekwisha kuanza katika eneo hilo na ambalo   Dkt Longopa alikuta vibarua wanaendelea na kazi ni pamoja na uchimbaji wa msingi.